Wanaume thelathini na tisa walihamishwa kwenye chombo mnamo Agosti lakini baadaye waliondolewa baada ya bakteria ya Legionella kupatikana kwenye mfumo wa maji wa bodi. Picha: Reuters

Wahamiaji ambao walikuwa wameondolewa na serikali ya Uingereza kutoka kwa mashua ya Bibby Stockholm mnamo Agosti baada ya kugunduliwa kwa bakteria ya Legionella watarejeshwa kwenye meli wiki ijayo, ripoti za vyombo vya habari zilisema.

''Wanaotafuta hifadhi wanaarifiwa na Ofisi ya Mambo ya Ndani ya Uingereza kwamba watarudishwa kwenye jahazi la wahamiaji lililowekwa katika Bandari ya Portland huko Dorset kusini-magharibi mwa nchi hiyo,'' BBC iliripoti Jumanne.

Katika barua, wanaotafuta hifadhi waliambiwa "utahitajika kuhamia makazi mbadala, na haswa, mashua ya Bibby Stockholm," na kwamba "makazi haya yanatolewa kwa msingi wa kutokuwa na chaguo."

Barua ya Ofisi ya Mambo ya Ndani inasema wahamiaji hao watarejeshwa kwenye jahazi mnamo Oktoba 19, ripoti hiyo iliongeza.

Wanaume 39 walihamishwa kwenye chombo mnamo Agosti lakini baadaye waliondolewa kwenye jahazi baada ya bakteria ya Legionella kupatikana kwenye mfumo wa maji wa bodi.

Sera ya Uingereza ya kudhibiti Uhamiaji imekumbwa na shutuma za ukiukaji wa haki za binadamu, japo serikali inasisitiza kuwa ndio nji ay apekee ya kuangamiza uhamiaji haramu nchini humo.

Maamuzi ya mahakama yanasubiriwa

Mbali na kuwafungia wanaotafuta hifadhi katika boti hilo, kuna mpango pia wa kuwahamishia nchini Rwanda ambako watazuiliwa kwa muda wakiendelea na utaratibu wa kuchunguzwa uhalali wao na kutafutiwa sehemu ya hifadhi.

Lakini pia kuna uwezekano mkubwa wa kukosa kupelekwa kwingine na waachwe kuishi nchini Rwanda na kutangamana na jamii huku wakipewa mafunzo ya kiufundi kuendeleza maisha yao wakiwa huko.

Mpango huu utaigharimu serikali ya Uingereza zaidi ya doma milioni 150.

Hata hivyo hii imekashifiwa na wakereketwa wahaki za kibinadamu wanaosema kuwa Rwanda sio nchi muafaka ya kutoa hifadhi kwa wakimbizi kwani haina rekodi safi ya kulinda haki za binadamu, tamko ambalo limepingwa vikali na Rwanda.

Sera hiyo ilisitishwa kwa kubatilishwa na mahakama ya Uingereza, lakini sasa imerejeshwa tena mahakamani kwa rufaa ya serikali ya Uingereza ambayo bado inataka kuitekeleza.

Rufaa hiyo iliyoanza kusikilizwa Jumanne 10 Oktoba itaendelea kwa siku tatu , kisha uamuzi unatarajiwa kutolewa na mahakama hiyo kabla kumalizika mwaka.

TRT Afrika