| Swahili
AFRIKA
2 DK KUSOMA
Uganda yazindua ujenzi wa reli inayojengwa na kampuni ya Uturuki
Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ameongoza uzinduzi wa reli ya kisasa ya SGR, mradi unaotekelezwa na kampuni ya Yapi Merkezi kutoka Uturuki.
Uganda yazindua ujenzi wa reli inayojengwa na kampuni ya Uturuki
Mradi huo unatarajiwa kuchochea biashara kati ya Uganda na nchi majirani./Picha: Yoweri Museveni       / Others
21 Novemba 2024

Rais wa Uganda Yoweri Museveni, siku ya Alhamisi amezindua ujenzi wa mradi wa reli ya kisasa (SGR), mradi unaotekelezwa na kampuni ya Uturuki ya Yapi Merkezi.

Pindi utakapokamilika, reli hiyo itakuwa na uwezo wa kusafirisha tani 1,000 za mzigo kwa wakati mmoja.

Kulingana na Rais Museveni, mradi huo utachochea biashara kati ya Uganda na nchi nyingine za jirani pamoja na sekta zingine za kiuchumi.

"Kiwango cha biashara barani Afrika kinashuka kwa asilimia 40 kutokana na ubovu wa miundombinu, huku gawio lake likiwa chini ya asilimia 15 wakati kwa mabara mengine inafikia asilimia 40 hadi 60," alisema Rais Museveni.

Kuchochea biashara ya kanda

Museveni amesema kuwa kutokuunganika vizuri kwa miondombinu barani Afrika, kunatatiza biashara, na hivyo kulifanya bara hilo kuendelea kutegemea masoko ya nje.

"Kwa kuunganisha Uganda na ukanda wote, tunaazimia kuchochea biashara ya kikanda, huku tukifanya biashara ndani ya Afrika," aliongeza.

Kwa mujibu wa Rais Museveni, usafiri kati ya Mombasa na Kampala utatumia saa 10, tofauti na saa 14, pindi mradi huo utakapokamilika.

Kwa upande wake, Balozi wa Uturuki nchini Uganda, Fatih Ak, alisema kuwa Ankara itaendelea kuunga mkono ajenda ya maendeleo ya Uganda.

Pata habari zaidi kupitia Whatsapp channels

CHANZO:TRT Afrika