Tanzania leo hii inaadhimisha kilele cha mapambano dhidi ya ugonjwa wa Marburg. Picha Wizara ya Afya Tanzania

Katika kilele cha mapambano dhidi ya ugonjwa wa Marburg nchini Tanzania serikali ya nchi hiyo kupitia mganga mkuu wa serikali imesema mpaka kufikia mei 31 imekuwa na jumla ya wagonjwa 9 tu.

"Hadi kufikia tarehe 31 Mei, 2023 jumla ya watu waliopata maambukizi ni tisa (9), kati ya hao wagonjwa watatu (3) wamepona akiwemo daktari wa kituo cha Afya Maruku aliyewahudumia wagonjwa wa mwanzo", Mganga Mkuu wa Serikali Prof Tumaini Nagu alifafanua

Hata hivyo mtaalamu huyo aliongeza kuwa mpaka sasa Tanzania imepoteza wagonjwa 6 kutokana na ugonjwa huo akiwemo mtoto wa miezi 18.

"Wagonjwa sita (6) walipoteza maisha akiwemo mtaalamu wa maabara kutoka Kituo cha Afya Maruku na mtoto mwenye umri wa miezi 18 ambaye mama yake ni miongoni mwa wagonjwa waliopona.

Hata hivyo Tanzania imebainisha kuwa mara ya mwisho kuwa na mgonjwa wa marburg ilikua ni mwezi April. Na ilipofika juzi tarehe 31 Mei 2023, nchi hiyo lifikisha siku 42 tangu mgonjwa wa mwisho kupona Virusi vya Marburg

"Mgonjwa wa mwisho alibainika kuwa hana maambukizi (Negative) tarehe 19 Aprili 2023" hivyo tulifikisha siku 42 tangu mgonjwa wa mwisho kupona Virusi vya Marburg, na kukidhi vigezo vya WHO vya kutangaza mwisho wa mlipuko wa ugonjwa wa Marburg".

"Kwa muktadha huu, leo tarehe 02 Juni 2023 ninatamka kuwa, mlipuko wa ugonjwa wa Marburg umekwisha rasmi” mganga mkuu wa Tanzania profesa Nagu alibainisha".

TRT Afrika