| Swahili
AFRIKA
2 DK KUSOMA
Shambulizi la anga jimboni Puntland laua zaidi ya wapiganaji 13 wa Daesh
Kulingana na vikosi vya ulinzi na usalama vya Puntland, magaidi hao waliuwawa wakati wa operesheni ya siku moja.
Shambulizi la anga jimboni Puntland laua zaidi ya wapiganaji 13 wa Daesh
Shambulio hilo linakuja zaidi ya wiki moja baada ya Kamandi ya Afrika ya Jeshi la Marekani (AFRICOM) kuthibitisha kutekeleza mashambulizi ya anga dhidi ya ISIS na Somalia./Picha: Wengine / Others
10 Februari 2025

Vikosi vya usalama nchini Somalia vimesema kuwa shambulizi la anga la hivi karibuni, limefanikiwa kuwauwa zaidi ya wapiganaji 13 wa vikundi vya Daesh na ISIS, katika eneo la Bari.

Katika taarifa yake iliyotolewa siku ya Jumatatu, shambulio hilo lililenga magaidi hao waliokuwa wamejificha, katika muendelezo wa mapambano dhidi ya wapiganaji, kulingana na maofisa wa usalama.

“Operesheni hiyo ilidumu kwa saa 24 na kufanikiwa kuua zaidi ya wapiganaji 13 katika eneo la Dhasaq, liliokuwa katika safu ya milima ya Calmiskaad,” kitengo cha kupambana na ugaidi cha Puntland kilisema siku ya Jumatatu.

Maofisa wa usalama pia wameendelea na operesheni zaidi katika eneo la Hararyo na Toga-Jeceel, hadi kuelekea kwenye ngome za Daesh/ISIS.

“Walifanikiwa kubaini ngome zilizokuwa zikitumika na vikundi vya kigaidi vya ISIS,” kilisema kitengo hicho kupitia taarifa yake kwenye ukurasa wa X.

Hata hivyo, vikosi hivyo vya usalama havikuweka wazi ni nchi gani iliyotekeleza shambulio hilo la anga.

Shambulio hilo linakuja zaidi ya wiki moja baada ya Kamandi ya Afrika ya Jeshi la Marekani (AFRICOM) kuthibitisha kutekeleza mashambulizi ya anga dhidi ya ISIS na Somalia.

Pata habari zaidi kupitia Whatsapp channels

CHANZO:TRT Afrika