Mwanamume akiondoa vifusi kwenye barabara iliyofurika baada ya watu kumi kufa katika kijiji cha Bupfune karibu na Kibuye, katika jimbo la magharibi mwa Rwanda Mei 4, 2023. Picha: AFP

Rwanda inahitaji angalau Rwf 130 bilioni ($116.2 milioni) kukarabati miundombinu muhimu iliyoharibiwa wakati wa mafuriko, waziri wa Usimamizi wa Dharura, Marie-Solange Kayisire, amesema.

Fedha hizo zitatumika kukarabati barabara, shule na vituo vya matibabu vilivyoharibiwa na mafuriko ya hivi majuzi na maporomoko ya ardhi yaliyogharimu maisha ya watu 131.

Zaidi ya nyumba 6,000 zilisombwa na mafuriko katika majimbo ya kaskazini, magharibi na kusini mwa Rwanda.

Kayisire alisema Jumamosi kuwa kiasi cha dola milioni 116.2 kilikuwa makadirio, na kwamba ripoti ya kina ya tathmini itafichuliwa baadaye.

Barabara kuu kumi na nne, zaidi ya shule 50 na madaraja kadhaa zilibeba mzigo mkubwa wa mafuriko.

Waziri wa Miundombinu Ernest Nsabimana alisema Rwf110 bilioni (dola milioni 98.3) zitatumika katika kujenga upya barabara za kitaifa na wilaya, madaraja, kurejesha uunganisho wa umeme na usambazaji wa maji.

"Madaraja yaliyoathiriwa yatalazimika kujengwa upya kwa sababu hatuwezi kuyakarabati," Nsabimana alisema Jumamosi wakati wa mkutano wa mawaziri na waandishi wa habari katika mji mkuu Kigali.

Aliongeza: "Tunahitaji kujenga miundombinu inayostahimili hali ya hewa ambayo inaweza kuhimili majanga kama yale tuliyopata hivi majuzi."

Hadi sasa, barabara tisa kati ya 14 zilizoharibika zimefunguliwa, alisema Nsabimana.

Idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko na maporomoko ya ardhi yaliyotokea Jumanne na Jumatano inafikia 131, serikali ilisema.

TRT Afrika