Ripoti  zilisema watu watano, wakiwemo washauri wa kijeshi wa Emarati, waliuawa katika shambulio hilo / Picha : AFP

Majeruhi wameripotiwa katika tukio la kupigwa risasi katika kambi ya mafunzo ya kijeshi katika mji mkuu wa Somalia wa Mogadishu, kulingana na maafisa.

Ufyatuaji risasi huo ulitekelezwa na "mjeshi" ambaye alifyatua risasi katika kituo cha kijeshi cha Jenerali Gordon siku ya Jumamosi, na kusababisha majeruhi kadhaa, chanzo cha usalama kililiambia shirika la habari la Anadolu kwa sharti la kutotajwa jina kutokana na vikwazo vya kuzungumza na vyombo vya habari.

Mshambuliaji huyo alifyatua risasi na kuwalenga washauri wa kijeshi wa Umoja wa Falme za Kiarabu kabla ya kupigwa risasi na vikosi vya usalama.

Idadi ya vifo na majeruhi bado haijajulikana lakini ripoti za vyombo vya habari zilisema watu watano, wakiwemo washauri wa kijeshi wa Emarati, waliuawa katika shambulio hilo.

Kwa mujibu wa Wizara ya Ulinzi ya UAE, wanajeshi watatu wa Imarati na afisa mmoja wa Bahrain waliuawa katika shambulio la kigaidi nchini Somalia.

Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamoud alilaani vikali "shambulio hilo baya."

Al Shabaab yadai kuhusika

Mohamoud alituma salamu za rambirambi kwa familia, watu na serikali ya UAE kwa vifo vya wale "waliokuja Somalia kushiriki katika kujenga upya jeshi letu la taifa."

Afisa wa jeshi la Somalia alisema kuwa mshambuliaji aliuawa kwa kupigwa risasi. / Picha: Kumbukumbu ya AFP

Ameviagiza vyombo vya usalama kuanzisha uchunguzi kuhusu shambulio hilo.

Kundi la kigaidi la Al Shabab lilidai kuhusika na shambulio hilo na kusema kuwa mmoja wa wavamizi wake ndiye aliyehusika na shambulio hilo.

Somalia imekuwa ikikabiliwa na ukosefu wa usalama kwa miaka mingi, huku vitisho vikuu vikitoka kwa Al Shabab na makundi ya kigaidi ya Daesh.

Tangu mwaka 2007, Al Shabab imekuwa ikipambana na serikali ya Somalia na Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Afrika nchini Somalia (ATMIS) -- ujumbe wa pande nyingi ulioidhinishwa na Umoja wa Afrika na kuamriwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Kundi hilo la kigaidi limeongeza mashambulizi tangu Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamoud, ambaye alichaguliwa kwa muhula wa pili mwaka 2022, kutangaza "vita vya kila namna" dhidi ya kundi hilo.

TRT Afrika