Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) imewateua viongozi wa zamani Uhuru Kenyatta kutoka Kenya, Olusegun Obasanjo kutoka Nigeria, na Hailemariam Desalegn kutoka Ethiopia kuwa wawezeshaji wa mpango wa pamoja wa amani unaolenga kutatua mzozo Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Uamuzi huo ulifikiwa wakati wa Mkutano wa ngazi ya juu wa Pamoja wa Wakuu uliofanyika jijini Dar es Salaam Februari 8, 2025, ulioongozwa na Rais wa Zimbabwe na Mwenyekiti wa SADC Emmerson Mnangagwa na Rais wa Kenya na Mwenyekiti wa EAC William Ruto.
Mkutano huo ulilenga kuimarisha juhudi za kikanda za kurejesha utulivu mashariki mwa DRC, ambayo imekuwa ikikumbwa na migogoro ya kivita inayoendelea.
Katika taarifa iliyochapishwa katika mtandao wa X, Rais William Ruto alisme Hatua hii inatarajiwa kuongeza juhudi za kidiplomasia, kuhakikisha jibu la ufanisi zaidi kwa mgogoro unaoendelea.
Mkutano wa viongozi wa kijeshi wa eneo
Kufuatia mkutano huo, mikutano ya maandalizi ilifanyika Nairobi Februari 21, ambapo Wakuu wa Majeshi ya Ulinzi ya EAC (CDFs) walijadili maagizo ya kimkakati ya kuimarisha amani.
Viongozi wa kijeshi wa SADC walikutana kando mjini Dar es Salaam kutathmini matatizo ya usalama katika kanda hiyo.
Mikutano hii iliandaa mazingira ya mkutano wa pamoja wa wakuu wa majeshi wa EAC na SADC uliopangwa kufanyika Februari 24, ukifuatiwa na Mkutano wa Pamoja wa Mawaziri Februari 28 kupitia maendeleo na kukubaliana juu ya hatua zaidi za usalama.
Vipaumbele muhimu vilivyoainishwa katika mkutano huo ni pamoja na kuweka usalama wa kutosha Goma na maeneo yanayoizunguka, kuwezesha misaada ya kibinadamu, kufungua tena njia muhimu za ugavi, na kutekeleza usitishaji mapigano mara moja.