Waandamanaji wa kupinga bili ya fedha wakabiliana na polisi jijini Nairobi / Picha: Reuters

Rais wa Kenya William Ruto ametangaza mabadiliko kwenye Muswada wa Fedha wenye utata ambao umesababisha maandamano katika mji mkuu wa taifa hilo.

Ruto na Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha Kimani Kuria waliwaelezea wabunge na maseneta mabadiliko yaliyofanywa kwenye muswada huo katika Ikulu ya Nairobi siku ya Jumanne.

Ruto alisema mabadiliko hayo yamezingatia maoni ya wananchi na wadau wengine wakati wa vikao vya ushirikishwaji wa umma.

"Tutaishia kuwa na kitu bungeni iliyotoka kwa Utawala na imechunguzwa na Bunge. Kupitia ushirikishwaji wa wananchi, raia wa Kenya wamepata nafasi ya kutoa maoni yao," alisema Ruto.

Nini Kimebadilika?

Muswada wa Fedha umerekebishwa ili kuondoa VAT iliyopendekezwa ya asilimia 16 kwenye mkate, usafirishaji wa sukari, huduma za kifedha, miamala ya fedha za kigeni, na ushuru wa asilimia 2.5 kwa magari.

Ruto aliongeza kuwa hakutakuwa na ongezeko la ada za uhamisho wa pesa kwa njia ya simu, na ushuru wa ziada kwenye mafuta ya mboga pia umeondolewa.

Ada za Mfuko wa Nyumba na ile iliyopendekezwa ya Bima ya Afya ya Kijamii pia hazitavutia kodi ya mapato.

"Ushuru wa Mazingira uliopendekezwa utawekwa tu kwenye bidhaa zilizokamilika zinazoagizwa kutoka nje ambazo zinachangia taka za kielektroniki na hivyo kuharibu mazingira zinapokuwa hazitumiki tena," alisema Ruto.

Mabadiliko ya Ushuru wa Mazingira

Bunge linapaswa kupitisha toleo la mwisho la muswada huo kabla ya Juni 30.

Kwa hivyo, bidhaa zinazotengenezwa nchini, zikiwemo taulo za kike, nepi, simu, kompyuta, tairi, na pikipiki, hazitavutia Ushuru wa Mazingira.

Rais alisisitiza kuwa serikali inafanya juhudi za kudhibiti uagizaji wa bidhaa zinazoweza kutengenezwa nchini, hivyo kulinda uzalishaji wa ndani na kuhifadhi ajira kwa watu.

Alisema Ushuru wa Mazingira utawekwa kwenye bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, wakati zile zinazotengenezwa nchini zitaachwa.

Hii inamaanisha bidhaa zinazotengenezwa nchini, zikiwemo taulo za kike, nepi, simu, kompyuta, tairi, na pikipiki, hazitavutia Ushuru wa Mazingira.

Usajili wa VAT

Kiwango cha usajili wa VAT pia kimeongezwa kutoka KSh5 milioni hadi KSh8 milioni, ikimaanisha biashara nyingi ndogo hazitahitaji tena kusajiliwa kwa VAT.

Serikali pia imetangaza kuwa mfumo wa ankara za kielektroniki ETIMS, ulioanzishwa hivi karibuni na Mamlaka ya Mapato ya Kenya, umefutwa kwa wakulima na biashara ndogo ndogo zenye mapato ya chini ya KSh1 milioni.

Rais Ruto alisema Utawala na Bunge vitaendelea kufanya kazi pamoja "katika kufanya maamuzi sahihi kwa nchi."

TRT Afrika