Balozi wa Marekani ndani ya Umoja wa Mataifa Linda Thomas-Greenfield (katikati) akipiga kura wakati wa kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu Gaza, katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa.  / Picha: AFP  

Wapatanishi lazima wahakikishiwe ahadi ya umma kutoka kwa Israeli ya kusitisha mapigano huko Gaza "ili tuweze kuingia katika mazungumzo," ofisa mkuu wa Hamas ameiambia TRT World.

"Na ni lazima Marekani iwe tayari kuwa mdhamini wa kila litakalokubaliwa," amesema ofisa huyo.

Masharti hayo yanakuja wakati Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limepitisha azimio la kwanza la kusitisha miezi nane ya vita vya Israeli katika eneo la Gaza.

Azimio hilo linalofadhiliwa na Marekani linakaribisha pendekezo la kusitisha mapigano lililotangazwa na Rais Joe Biden ambalo Marekani inadai Israeli imelikubali. Inatoa wito kwa kundi la Palestina la Hamas kukubali mpango huo wa awamu tatu. Tangu mpango huo kutangazwa maafisa wa Israeli akiwemo waziri mkuu Benjamin Netanyahu wamekuwa wakikataa yaliyomo ndani kwa visingizio tofauti.

Hamas imeonesha wasiwasi wake wa iwapo Israeli itaheshimu makubaliano na hivyo kutaka udhamini kutoka kwa mshirika mkubwa wa Israeli, Marekani.

Azimio hilo, lililopitishwa na wajumbe 14 kati ya 15 wa Baraza la Usalama, linazitaka Israeli na Hamas kulitekeleza "haraka iwezekanavyo na bila masharti yoyote."

Iwapo Israeli na Hamas watakubali kuendelea na mpango huo ama la, bado uungwaji mkono mkubwa wa azimio hilo katika chombo chenye nguvu zaidi cha Umoja wa Mataifa unaweka shinikizo la ziada kwa pande zote mbili kuidhinisha pendekezo hilo.

TRT Afrika